Pages

Ajali ya basi yajeruhi watu 30

May 14, 2012

Add caption
Watu 30 wamejeruhiwa huku wanane wakiwa mahututi baada ya basi la kampuni ya Zakaria Express, yenye namba za usajili T 982 ECJ aina ya Scania kupata ajali katika eneo la Kahangara wilayani Magu Mkoa wa Mwanza jana jioni.
Gari hilo lililobeba abiria zaidi ya 60 likitokea Mwanza kuelekea Tarime, mkoani Mara lilipata ajali likiwa katika mwendo wa kasi baada ya nati ya mguu wa kulia kukatika ghafla.
Majeruhi wa ajali hiyo walipelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Magu kwa matibabu zaidi na wengine wawili kukimbizwa katika Hospitali ya Rufani ya Bugando kutokana na hali zao kuwa mbaya.
Katika hali ya kushangaza, wakazi wa eneo la Kahangara badala ya kusaidia kuokoa majeruhi wa ajali hiyo, waliwavamia majeruhi hao na kuwaibia mizigo yao pamoja na fedha.
Hadi polisi wanafika katika eneo la tukio, majeruhi wengi walikuwa wanalalamika kwa kupoteza baadhi ya mali zao na kuwatuhumu vijana waliowavamia na kuwanyang’ang’anya mizigo yao. Aidha, dereva wa basi hilo alikimbia baada ya ajali.
Jitihada za kumpata Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Deuxdedit Nsimeki, kuelezea chanzo cha tukio hilo zilishindikana kutokana na kutopatikana katika simu yake ya mkononi.
SOURCE: NIPASHE