Pages

UKIBAKWA USIOGE: MADAKTARI

May 9, 2012



MADAKTARI wamehadharisha watu wanaobakwa kwamba wakishatendwa hivyo wasioge au kubadili nguo kwa sababu kufanya hivyo kunapoteza ushahidi muhimu wa kumtia hatiani kisheria mbakaji. 


Imeelezwa kuwa mtu akibakwa, anapaswa kwenda Polisi haraka kupata fomu namba tatu (PF3) na awahishwe hospitali ya wilaya ambako atapewa matibabu ikiwa ni pamoja na dawa ya kuzuia maambukizi ya virusi vya ukimwi (VVU). 


Dawa ya kuzuia maambukizi ya VVU inayojulikana kama PEP, inaweza kufanya kazi endapo tu mwathirika atapewa ndani ya saa 72 baada ya kubakwa kama kabla ya kubakwa hakuwa na maambukizi. 


Akizungumza jana na wanahabari walioshiriki utafiti wa masuala ya ukatili wa kijinsia uliofanywa na Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) wilayani Kinondoni, Dar es Salaam, Dk. Zuberi Mzige wa hospitali ya Mwananyamala, alisema watoto, wasichana na wanawake wengi wanaofika hospitalini baada ya kubakwa na kunajisiwa, huwa wamepoteza ushahidi kwa kuoga na kubadili nguo walizovaa wakati wakibakwa. 
Aidha, alisema wengi hufika hospitalini wamechelewa na hivyo kuwa katika hatari kubwa ya kupata maambukizi ya VVU. 


Alisema kesi nyingi za ubakaji zimekuwa zikikosa ushahidi wa madaktari, kwa sababu aliyebakwa anatakiwa kupelekwa hospitalini akiwa na nguo zake na ‘uchafu’, kwa sababu ushahidi wa Polisi na daktari kuwa tendo la ubakaji limefanyika ni nguo alizobakwa nazo mwathirika. 


Dk. Prisca Berege anayeshughulika na magonjwa ya watoto Mwananyamala, alisema lipo tatizo kubwa la kunajisi watoto Dar es Salaam na kwamba hatua zisipochukuliwa, Taifa litapata madhara makubwa. 


Dk. Berege alisema, kwa wastani kila siku hospitali hiyo hupokea watu watatu waliobakwa au kunajisiwa, ambao ni wanawake na watoto, na vitendo vingi vya ubakaji huripotiwa hospitalini hapo usiku, hivyo aliasa wazazi kuepuka kutuma watoto wao usiku. 


Aidha, alihadharisha wasichana kuepuka kwenda kwenye nyumba za wanaume hata kama wanawaamini na ni marafiki zao, kwani baadhi ya wanaume huwa na nia mbaya ya kubaka hata mchana. 


Alitoa mfano wa binti ambaye hivi karibuni alibakwa mchana kwenye nyumba ya mwanamume aliyemwamini na kumthamini kama kaka yake na mwajiri wake. 


Mwanamume huyo alimwita nyumbani kwa kumdanganya kuwa kuna kazi wangekwenda kupanga kufanya na kisha kumgeuka.